Date: 
20-08-2024
Reading: 
Isaya 8:11-15

Jumanne asubuhi tarehe 20.08.2024

Isaya 8:11-15

11 Maana Bwana aliniambia hivi, kwa mkono hodari, akanifundisha nisiende katika njia ya watu hawa, akisema,

12 Msiseme, Ni fitina, katika habari za mambo yote ambayo watu hawa watasema, Ni fitina; msihofu kwa hofu yao, wala msiogope.

13 Bwana wa majeshi ndiye mtakayemtakasa; na awe yeye hofu yenu, na awe yeye utisho wenu.

14 Naye atakuwa ni mahali patakatifu; bali ni jiwe la kujikwaza na mwamba wa kujikwaa kwa nyumba za Israeli zote mbili, na mtego na tanzi kwa wenyeji wa Yerusalemu.

15 Na wengi watajikwaa juu yake, na kuanguka na kuvunjika, na kunaswa na kukamatwa.

Nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari;

Tumeusoma ujumbe wa Bwana kwa Israeli kupitia kwa Nabii Isaya, kwamba wasiende katika njia ya uovu. Israeli wanatakiwa kuenenda katika njia ya Bwana wa majeshi, yeye anayeandikwa kuwa hofu na utisho. Hapa Isaya alimaanisha kuwa Bwana ndiye alikuwa mwanzo na mwisho kwa watu wake. Isaya anakazia kwamba Bwana ni Mtakatifu, hivyo watu wafuate njia yake tu.

Ujumbe huu walipewa wana wa Israeli kabla ya kuvamiwa na Ufalme wa Ashuru, na baadaye kuwa mateka Babeli. Walitakiwa kuishi katika njia ya Bwana ili kuiepuka ghadhabu ya Mungu. Kristo ametukomboa kwa njia ya kifo na kufufuka, hivyo tunaalikwa kumtegema yeye tukiwa wanyenyekevu ili tuwe na mwisho mwema. Amina

Jumanne njema

Heri Buberwa