Date: 
15-08-2024
Reading: 
Luka 9:57-62

Alhamisi asubuhi tarehe 15.08.2024

Luka 9:57-62

57 Nao walipokuwa wakienda njiani, mtu mmoja alimwambia, Nitakufuata ko kote utakakokwenda.

58 Yesu akamwambia, Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake.

59 Akamwambia mwingine, Nifuate. Akasema, Bwana, nipe ruhusa kwanza niende nikamzike baba yangu.

60 Akamwambia Waache wafu wawazike wafu wao; bali wewe enenda ukautangaze ufalme wa Mungu.

61 Mtu mwingine pia akamwambia, Bwana, nitakufuata; lakini, nipe ruhusa kwanza nikawaage watu wa nyumbani mwangu.

62 Yesu akamwambia, Mtu aliyetia mkono wake kulima, kisha akaangalia nyuma, hafai kwa ufalme wa Mungu.

Mtafuteni Bwana nanyi mtaishi;

Yesu anafundisha kuhusu wafaao kuwa wanafunzi wake. Kuna aliyemwambia Yesu nitakufuata kokote utakakokwenda, Yesu akamwambia Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake. Ukiangalia unaona kama Yesu anasema hana mahali pa kulaza hata kichwa chake. Yesu hapa alikuwa anamwambia huyu ndugu kwamba kumfuata Yesu haikuwa kazi nyepesi.

Mwingine aliitwa amfuate Yesu, lakini akaomba ruhusa kwanza akamzike baba yake. Yesu akamwambia awaache wafu wawazike wafu wao, bali yeye akautangaze ufalme wa Mungu. Haimaanishi usishiriki maziko, bali maisha yetu yasitufanye tumuache Yesu.

Mwingine alitaka kumfuata Yesu, lakini aliomba ruhusa akawaage ndugu zake. Yesu anamwambia kuwa aliyetia mkono wake kulima akaangalia nyuma hafai kwa ufalme wa Mungu. Hapa Yesu alimaanisha kwamba mtu akiamua kumfuata amfuate kwelikweli, asiangalie nyuma

Ukiangalia ndugu wote watatu tuliowasoma walitaka kumfuata Yesu, lakini bado kuna mambo walitaka kukamilisha. Mfano huu unatukumbusha kuwa imara katika njia ya ufuasi wetu, na kuwa makini katika njia zetu ili tusimuache Kristo. Tuzingatie maisha yetu kuwa ya kumcha Bwana, na kubaki katika njia yake wakati wote. Tunabaki kwa Bwana tukimwamini na kumtegemea. Amina

Alhamisi njema

Heri Buberwa