Date: 
22-04-2024
Reading: 
1Petro 1:16-21

Jumatatu asubuhi tarehe 22.04.2024

1 Petro 1:16-21

16 kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.

17 Na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni.

18 Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu;

19 bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo.

20 Naye amejulikana kweli tangu zamani, kabla haijawekwa misingi ya dunia; lakini alifunuliwa mwisho wa zamani kwa ajili yenu;

21 ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.

Maisha mapya ndani ya Kristo;

 Katika somo la asubuhi ya leo, Petro anaanza kwa kusema kuwa Imeandikwa mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni Mtakatifu. Hapa ni muhimu kurejea kuwa Petro alikuwa anarejea maandiko ya kale kama tunavyosoma;

Mambo ya Walawi 11:44-45

44 Kwa kuwa mimi ni Bwana, Mungu wenu; takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu; wala msitie uchafu nafsi zenu kwa kitu kitambaacho cha aina yo yote, kiendacho juu ya nchi.
45 Kwa kuwa mimi ni Bwana niliyewaleta kutoka nchi ya Misri, ili kwamba niwe Mungu wenu; basi mtakuwa watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.

Rejea nyingine za Petro;

Mambo ya Walawi 19:2

Nena na mkutano wote wa wana wa Israeli, uwaambie, Mtakuwa watakatifu; kwa kuwa mimi Bwana, Mungu wenu, ni mtakatifu.

Mambo ya Walawi 20:7

Jitakaseni basi, iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.

Petro alikuwa anatoa wito wa kuishi maisha ya Utakatifu, kwa kumwamini Kristo aliye na ahadi ya kuwafanya watu watakatifu kama yeye. Ndiyo maana ukiendelea kusoma unaona Petro akisema kuwa Kristo ndiye aliyewakomboa wanadamu kwa damu yake msalabani.

Kristo aliyekufa msalabani na kutukomboa kwa damu hutuita kumwamini na kumfuata, maana tukikaa katika yeye maisha yetu yanakuwa mapya siku zote. Amina.

Uwe na wiki njema yenye maisha mapya katika Kristo.

 

Heri Buberwa