Date: 
16-12-2022
Reading: 
Marko 1:4-8

Hii ni Advent 

Ijumaa asubuhi tarehe 16.12.2022

Marko 1:4-8

[4]Yohana alitokea, akibatiza nyikani, na kuuhubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi.

[5]Wakamwendea nchi yote ya Uyahudi, nao wa Yerusalemu wote, wakabatizwa katika mto wa Yordani, wakiziungama dhambi zao.

[6]Na Yohana alikuwa amevaa singa za ngamia na mshipi wa ngozi kiunoni mwake, akala nzige na asali ya mwitu.

[7]Akahubiri akisema, Yuaja nyuma yangu aliye na nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuinama na kuilegeza gidamu ya viatu vyake.

[8]Mimi niliwabatiza kwa maji; bali yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu.

Bwana anawafariji watu wake;

Yohana Mbatizaji mjumbe wa Bwana alimtangulia Yesu akitangaza ujio wake (Yesu). Alihubiri ubatizo wa toba kwa ondoleo la dhambi. Alikazia kuwa watu waandae mioyo kumpokea Yesu ajaye, maana alikuwa anakuja kwa watu wake, na Yohana alisema huyu Yesu ni mkuu kuliko yeye. Kwa maana hiyo Yohana alimtambulisha Yesu kama Mfalme.

Ujumbe wa Yohana unatukumbusha kujiandaa kumpokea Yesu. Kujiandaa kumpokea Yesu ni kuishi maisha yanayompendeza, tukitenda yatupasayo. Maisha yetu yawe yenye ushuhuda wa Kikristo, tunapongojea kurudi kwake, maana akija atatulipa kila mmoja kwa kadri ya matendo yake.

Siku njema.