Date: 
28-09-2023
Reading: 
Hesabu 22:1-14

Alhamisi asubuhi 28.09.2023

Hesabu 22:1-14

1 Kisha wana wa Israeli wakasafiri na kupanga katika nchi tambarare za Moabu ng'ambo ya pili ya Yordani karibu ya Yeriko.

2 Na Balaki mwana wa Sipori akaona mambo yote ambayo Israeli wamewatendea Waamori.

3 Moabu akawaogopa hao watu sana, kwa kuwa walikuwa wengi; Moabu akafadhaika kwa sababu ya wana wa Israeli.

4 Moabu akawaambia wazee wa Midiani, Sasa jeshi hili la watu litaramba vitu vyote vinavyotuzunguka, kama vile ng'ombe arambavyo majani ya mashamba. Na Balaki, mwana wa Sipori, alikuwa mfalme wa Moabu zamani zile.

5 Basi akatuma wajumbe kwa Balaamu mwana wa Beori, hata Pethori, ulio kando ya Mto, mpaka nchi ya wana wa watu wake, kwenda kumwita, akisema, Tazama, kuna watu waliotoka Misri; tazama, wanaufunika uso wa nchi, tena wanakaa kunikabili mimi.

6 Basi, njoo wewe, nakusihi unilaanie watu hawa; maana wana nguvu kunishinda mimi. Labda nitawaweza, tupate kuwapiga, niwafukuze watoke katika nchi yangu, kwa maana najua ya kuwa yeye umbarikiye hubarikiwa, na yeye umlaaniye hulaaniwa.

7 Wazee wa Moabu, na wazee wa Midiani, wakaenda, wakichukua ujira wa uganga mikononi mwao; wakamfikilia Balaamu, wakamwambia maneno ya Balaki.

8 Akawaambia, Kaeni hapa usiku huu, nami nitawaletea jawabu kama Bwana atakavyoniambia; wakuu wa Moabu wakakaa na Balaamu.

9 Mungu akamjia Balaamu, akasema, Ni watu gani hawa ulio nao pamoja nawe?

10 Balaamu akamwambia Mungu, Balaki mwana wa Sipori, mfalme wa Moabu, amewatuma kwangu, akisema,

11 Tazama, kuna watu waliotoka Misri, wanaufunika uso wa nchi; basi njoo unilaanie watu hawa; labda nitaweza kupigana nao, na kuwafukuza.

12 Mungu akamwambia Balaamu, Usiende pamoja nao; wala usiwalaani watu hawa, maana wamebarikiwa.

13 Balaamu akaondoka asubuhi akawaambia wakuu wa Balaki, Enendeni zenu hata nchi yenu; kwa maana Bwana amekataa kunipa ruhusa niende pamoja nanyi.

14 Wakuu wakaondoka wakaenda kwa Balaki, wakasema, Balaamu, anakataa kuja pamoja nasi.

Mungu amejaa huruma;

Israeli wakiwa njiani kuelekea nchi ya ahadi walipita katika nchi ya Waamori bila shida, hadi kuwafukuza kwenye nchi yao. Sasa tumesoma wakiwa katika nchi ya Waamori. Kwa sababu ya kuwaogopa Waisraeli, wakuu wa Waamori wanaenda kuomba msaada kwa Balaamu ili awasaidie kuwaondosha. Balaamu aliambiwa na Mungu asishiriki kuwafanya lolote wana wa Israeli maana wamebarikiwa.

Hii ni sehemu tu ya yaliyowatokea wana wa Israeli wakiwa njiani kuelekea Kanaani. Mungu alikuwa upande wao, ndio maana alisema wamebarikiwa (12). Sisi nasi tunabarikiwa kwa njia ya Imani, pale tunapomwamini Yesu na kulishika neno lake. Mwamini Yesu uokolewe. Amina.

Alhamisi njema.

 

Heri Buberwa