Date: 
04-08-2023
Reading: 
Luka 15:8-10

Ijumaa asubuhi tarehe 04.08.2023

Luka 15:8-10

8 Au kuna mwanamke gani mwenye shilingi kumi, akipotewa na moja, asiyewasha taa na kufagia nyumba, na kutafuta kwa bidii hata aione?

9 Na akiisha kuiona, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimeipata tena shilingi ile iliyonipotea.

10 Nawaambia, Vivyo hivyo kuna furaha mbele ya malaika wa Mungu kwa ajili ya mwenye dhambi mmoja atubuye.

Wema wa Mungu watuvuta tupate kutubu;

Mfano huu ulio kwa njia ya swali unatanguliwa na mfano wa mtu mwenye kondoo mia, akapotea mmoja, halafu mtu huyo akawaacha tisini na tisa amtafute yule mmoja. Hapa tunamsoma mwanamke anayeitafuta shilingi moja hadi aipate, ijapokuwa amebaki na shilingi tisa. Hata ile shilingi moja ni muhimu.

Mifano yote miwili ni picha ya Mungu wetu aliye mwema, kwamba yeye huwa hapendi hata mmoja wetu apotee, bali wote watubu kama Petro anavyoandika;

2 Petro 3:9

Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.

Lengo la Mungu ni kila mmoja wetu atubu dhambi na kuokolewa. Tusipotubu tunakuwa tumepotea, kinyume na mapenzi ya Mungu. Tunaalikwa kuishi maisha ya toba wakati wote. Amina.

Ijumaa njema.

 

Heri Buberwa