Date: 
24-07-2023
Reading: 
Mithali 25:26-28

Jumatatu asubuhi tarehe 24.07.2023

Mithali 25:26-28

26 Mwenye haki amwangukiapo mtu mbaya Ni kama chemchemi iliyochafuka, Na kisima kilichokanyagwa.

27 Haifai kula asali nyingi mno; Vile vile mtu kutafuta utukufu wake mwenyewe si utukufu.

28 Asiyetawala roho yake Ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.

Uchaguzi wa busara;

Tunalianza Juma hili kwa kumsoma Suleimani kuhusu haki, kwamba mwenye haki akiangukia kwa mtu mbaya ni kama chemchemi iliyochafuka, ni sawa na kisima kilichokanyagwa. Hapa Suleimani anaangazia umuhimu wa mtu kubaki katika njia ya haki wakati wote mbele za Mungu. Mfalme Suleimani anamalizia kwa kusema kuwa asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, yaani kumuacha Bwana ni sawa na kupotea.

Haki ya Mungu anayotueleza Suleimani ni kuchagua kuishi maisha ya imani bila kuiacha. Tunaalikwa kudumu katika haki kwa njia ya imani kwa unyenyekevu mbele za Mungu mwenye Utukufu wote. Tusiruhusu roho zetu kuwa kama ukuta uliobomolewa, yaani tusimuache Bwana. Kudumu katika Imani ya kweli ndiyo Uchaguzi wa busara kuelekea uzima wa milele. Amina.

Uwe na wiki njema.

Heri Buberwa