Date: 
07-08-2024
Reading: 
Luka 12:44-48

Jumatano asubuhi tarehe 07.08.2024

Luka 12:44-48

44 Kweli nawaambia, atamweka juu ya vitu vyake vyote.

45 Lakini, mtumwa yule akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia kuja, akaanza kuwapiga wajoli wake, wanaume kwa wanawake, akila na kunywa na kulewa;

46 bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wasioamini.

47 Na mtumwa yule aliyejua mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana.

48 Na yule asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi.

Enendeni kwa hekima;

Yesu alikuwa akifundisha juu ya mtumwa mwaminifu na mtumwa asiye mwaminifu. Ukisoma kabla ya somo unaona hivi;

Luka 12:42-43

42 Bwana akasema, Ni nani, basi, aliye wakili mwaminifu, mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya utumishi wake wote, awape watu posho kwa wakati wake?
43 Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo.

Unaona Yesu anauliza nani wakili mwaminifu ambaye bwana wake atamweka juu ya wote atende ipasavyo, na anasema ana heri ikiwa atatenda vema bwana wake ajapo.

Ndipo Yesu anaendelea katika somo akisema kuwa bwana arudipo atamweka juu ya vyote. Lakini Yesu anasema asipotenda ipasavyo, bwana wake atamkata vipande viwili na kumweka fungu moja na wasioamini. Anaendelea kusema kuwa yule ajuaye mapenzi ya bwana wake asiyatende atapigwa sana.

Yesu alitumia mfano wa uaminifu kwa watumwa (wakili) kuonesha uaminifu unavyotakiwa kwa waliompokea hadi atakaporudi. Yaani alikuwa anafundisha kuhusu kumcha yeye pasipo kuacha njia yake hata mwisho. Tunakumbushwa kuwa waaminifu hadi Bwana ajapo, yaani kusimama kwa Imani yetu hata mwisho ili tupate taji ya uzima. Amina

Jumatano njema.

Heri Buberwa